“ROZARI YA BIKIRA MARIA”

BARUA YA KITUME
 
“ROZARI YA BIKIRA MARIA”
 
YA BABA MTAKATIFU YOHANE PAULO II
KWA MAASKOFU, MAKLERI NA WAAMINI WOTE
KUHUSU ROZARI TAKATIFU
 
 
 
 
 

UTANGULIZI

 
 
1.  Rozari ya Bikira Maria, iliyostawi hatua kwa hatua katika milenia ya pili kwa uvuvio wa Roho wa Mungu,  ni sala iliyopendwa na watakatifu wengi na kuhimizwa na Ualimu wa Kanisa. Katika usahili na udhati wake inazidi kuwa sala muhimu sana, na kutarajiwa kuzaa matunda ya utakatifu katika milenia hii ya tatu iliyoanza tu. Yenyewe inafaa kuchangia safari ya Kiroho ya Ukristo ambao, baada ya miaka elfu mbili, haujapotewa na uhai wa asili yake na unajisikia kusukumwa na Roho wa Mungu kwenda kilindini ili kumtangaza tena kwa sauti kubwa Kristo kwa ulimwengu kuwa ndiye Bwana na Mwokozi, "njia, ukweli na uzima" (Yoh 14:6), "lengo la historia yote, kiini cha vipeo vya historia na cha ustaarabu wa binadamu". Kwa kuwa Rozari, ingawa ina sura ya Kimaria, ni sala ambayo moyo wake ni Kristo. Katika usahili wa sehemu zinazoiunda, inajumlisha ndani mwake udhati wa ujumbe wote wa Injili, ambao Rozari ni kama muhtasari wake. Ndani mwake mna mwangwi wa sala ya Maria, Magnificat, wimbo wake usiopitwa na wakati kwa ajili ya umwilisho wenye kulenga ukombozi wa watu ulioanza katika tumbo lake la kibikira. Kwa njia yake taifa la Wakristo linataka kujifunza kwa Maria, ili liingizwe hata kuzama ndani ya uzuri wa uso wa Kristo na kung'amua ukuu wa upendo wake. Kwa njia ya Rozari mwamini anachota wingi wa neema, kama kwa kuupokea mikononi mwa Mama wa Mkombozi.
 

Maaskofu wa Roma na Rozari

 
2. Sala hiyo ilitiwa maanani sana na watangulizi wangu wengi. Kuhusu jambo hilo anastahili kukumbukwa kwa namna ya pekee Leo XIII ambaye tarehe 1 Septemba 1883 alitoa barua rasmi Supremi Apostolatus Officio, tamko kuu ambalo lilifungua njia ya mengine mengi kuhusu sala hiyo aliyoielekeza kama chombo cha Kiroho cha kufaa dhidi ya maovu mengi ya jamii. Kati ya Baba Watakatifu wa mwishomwisho ambao wakati wa Mtaguso walijitokeza kuhamasisha Rozari napenda kuwataja mwenye heri Yohane XXIII na hasa Paulo VI ambaye katika himizo la kitume Marialis Cultus, akifuata mwelekeo wa Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikano, alisisitiza jinsi Rozari ilivyo na tabia ya Kiinjili na inavyomlenga Kristo. Halafu mimi mwenyewe sijaacha nafasi ya kuhimiza kusali Rozari mara nyingi. Tangu ujana wangu sala hiyo imeshika nafasi muhimu katika maisha yangu ya Kiroho. Safari yangu ya mwisho huko Polandi, na hasa ziara yangu katika patakatifu pa Kalwaria, imenikumbusha kwa nguvu jambo hilo. Rozari imenisindikiza katika furaha na katika majaribu. Kwake nilikabidhi mahangaiko mengi, kwake nikapata daima faraja. Miaka ishirini na minne iliyopita, tarehe 29 Oktoba 1978, wiki mbili tu baada ya kuchaguliwa nikalie ukulu wa Petro, kama kwa kuifungua roho yangu nilisema hivi: “Rozari ndiyo sala yangu pendevu kuliko zote. Sala nzuri ajabu! Ya ajabu katika usahili wake na udhati wake… Tunaweza kusema kwa namna fulani Rozari ni sala inayofafanua sura ya mwisho ya hati Lumen Gentium ya Mtaguso wa pili wa Vatikano, sura inayohusu uwepo wa ajabu wa Mama wa Mungu katika fumbo la Kristo na la Kanisa. Kwa maana juu ya maneno ya Salamu Maria yanapita mbele ya macho ya roho matukio makuu ya maisha ya Yesu Kristo. Yenyewe yameunda umoja wa mafumbo ya furaha, uchungu na utukufu, na kutuunganisha kwa namna hai na Kristo kupitia - tuseme - moyo wa Mama yake. Wakati huohuo moyo wetu unaweza kujumlisha katika makumi hayo ya Rozari matukio yote yanayounda maisha ya mtu binafsi, familia, taifa, Kanisa na binadamu kwa
jumla. Matukio ya binafsi na ya jirani na hasa ya wale ambao tunahusiana nao zaidi na kuwapenda zaidi. Hivyo sala sahili ya Rozari inalingana na madundo ya maisha ya binadamu". Kwa maneno hayo, wapendwa ndugu zangu, niliingiza katika mwendo wa kila siku wa Rozari mwaka wangu wa kwanza kama askofu wa Roma. Leo, mwanzoni mwa mwaka wa ishirini na tano wa huduma hiyo kama mwandamizi wa Petro, nataka kufanya vilevile. Jinsi zilivyo nyingi neema nilizozipokea miaka hiyo kwa Bikira Maria kupitia Rozari: Magnificat anima mea Dominum! Nataka kumuinulia Bwana shukrani zangu kwa maneno ya Mama yake mtakatifu, ambaye chini ya ulinzi wake nimeweka huduma yangu ya Kipapa: Totus tuus!
 

Oktoba 2002 - Oktoba 2003: mwaka wa Rozari

 
3. Kwa hiyo, kufuatana na tafakuri niliyoitoa katika barua ya kitume Novo Millennio Ineunte, ambamo nilialika taifa la Mungu "tuanze upya na Kristo" baada ya mang'amuzi ya jubilei kuu, nimejisikia haja ya kuandika tafakuri juu ya Rozari kama taji la Kimaria la barua hiyo, ili nihimize tuutazame uso wa Kristo tukiwa na Mama yake mtakatifu na tukijifunza kwake. Kwa sababu kusali Rozari ni hicho tu: kuutazama uso wa Kristo pamoja na Maria. Ili nitie maanani mwaliko huo, nikichukua fursa ya kutimia hivi karibuni kwa miaka 120 tangu Leo XIII atoe hati hiyo, nataka sala hiyo ipendekezwe na kutumiwa kwa namna ya pekee kwa muda wa mwaka mzima katika jumuia mbalimbali za Kikristo. Kwa hiyo nautangaza mwaka unaoanza Oktoba ya mwaka huu hadi Oktoba ya mwaka 2003 uwe mwaka wa Rozari. Nakabidhi elekezo hilo la kichungaji kwa bidii ya kila jumuia ya Kanisa. Kwa kufanya hivi sitaki kuvuruga, bali kukamilisha na kuimarisha mipango ya kichungaji ya Makanisa maalumu. Natumaini litapokewa kwa juhudi na utayari. Rozari ikivumbuliwa tena katika maana yake yote inafikisha hadi kiini chenyewe cha maisha ya Kikristo na kutoa nafasi ya kawaida yenye kuzaa matunda ya Kiroho na ya kimalezi kwa sala hasa, kwa malezi ya taifa la Mungu na kwa uinjilishaji mpya. Napenda kusisitiza hilo nikikumbuka kwa furaha tarehe nyingine, yaani kutimia miaka arubaini tangu uanze Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikano (11 Oktoba 1962), ambao ndio "neema kuu" iliyoandaliwa na Roho wa Mungu kwa Kanisa la nyakati zetu.

 

Hoja dhidi ya Rozari

 
4. Kwamba mwaka wa Rozari unafaa inatokana na kuzingatia mambo mbalimbali. La kwanza linahusu haja ya haraka ya kupambana na tatizo la sala hiyo kupuuziwa pasipo sababu katika hali ya sasa ya historia na ya teolojia na hivyo kutopendekezwa vya kutosha kwa vizazi vipya. Baadhi wanadhani kwamba nafasi ya kwanza inayoistahili liturujia, kama ilivyosisitizwa na Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikano, inadai kupunguza umuhimu wa Rozari. Kumbe, alivyoeleza Paulo VI, sala hiyo haipingani na liturujia, bali inaitegemeza, kwa kuwa inaiandaa na kuiitikia vema, ikiwezesha kuishiriki kabisa kwa dhati na kuyachuma matunda yake katika maisha ya kila siku.
Labda kuna wengine pia ambao wanaogopa kwamba sala hiyo haisaidii ekumeni, kutokana na tabia yake ya Kimaria hasa. Kumbe Rozari inajipanga katika mandhari safi zaidi ya ibada kwa Mama wa Mungu kadiri Mtaguso ulivyoichora: yaani ibada inayomlenga Kristo, kiini cha imani yetu, hivi kwamba "Mama anapoheshimiwa, Mwana ajulikane na kupendwa na kutukuzwa ipasavyo". Rozari, ikieleweka upya inavyofaa, ni msaada, sio kizuio kwa umoja wa Wakristo!
 

Njia ya sala hasa

 
5. Lakini sababu muhimu zaidi inayonifanya nipendekeze tena kwa nguvu matumizi ya Rozari ni kwamba yenyewe ni njia ya kufaa sana kwa kuwahamasisha waamini kuhusu ile juhudi ya kuzama katika fumbo la Kristo niliyoipendekeza katika barua ya kitume Novo Millennio Ineunte kama njia halisi ya 'malezi ya utakatifu' : "Tunahitaji aina ya Ukristo ambayo inajitokeza kwanza katika utaalamu wa kusali".  Wakati ambapo katika utamaduni wa kisasa, ingawa kati ya matata mengi, inaelea haja mpya ya maisha ya Kiroho, inayochochewa hata na athari za dini nyingine, kuna haja ya haraka kuliko siku za nyuma ya kuwa jumuia zetu za Kikristo zigeuke "shule halisi za sala".
Rozari inajipanga katika mapokeo bora na yenye mang'amuzi mengi zaidi ya sala hasa ya  Kikristo. Ikiwa imestawi huku Magharibi, ni sala yenye tabia ya kutafakari hasa na inalingana kwa namna fulani na "sala ya moyo" au "sala ya Yesu" iliyochipuka kwenye rutuba ya Mashariki ya Kikristo.

 

Sala kwa ajili ya amani na ya familia

 
6. Nafasi nyingine za historia ya leo zinaongeza sababu za kueneza upya Rozari siku hizi. Ya kwanza ni haja ya haraka ya kumsihi Mungu atujalie amani. Mara nyingi watangulizi wangu na mimi mwenyewe tuliipendekeza Rozari kama sala kwa ajili ya amani. Mwanzoni mwa milenia mpya, ambayo ilianza na matukio ya kutisha ya mauaji ya tarehe 11 Septemba 2001 na ambayo inarekodi kila siku katika sehemu mbalimbali za dunia nafasi mpya za umwagaji damu na ukatili, kuvumbua upya Rozari ni kuzama katika fumbo la yule ambaye "ndiye amani yetu" kwa kuwa ametufanya "sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga" (Ef 2:14).  Kwa hiyo haiwezekani kusali Rozari bila ya kujisikia tunahusika na jukumu maalumu la kuhudumia amani, kwa namna ya pekee kwa ajili ya nchi ya Yesu, ambayo inazidi kupatwa na majaribu makali na inapendwa sana na moyo wa Wakristo.
Haraka hiyohiyo ya kuwajibika na kusali inajitokeza upande mwingine wenye utata wa wakati wetu, ule wa familia, seli ya jamii, inayozidi kushambuliwa na miundo inayobomoa kinadharia na kimaisha, hata kutia wasiwasi kuhusu kesho ya muundo huo wa msingi usiokanushika na kuhusu kesho ya jamii nzima pamoja nao. Kueneza upya Rozari katika familia za Kikristo, kama sehemu ya mpango mpana zaidi wa uchungaji wa familia, ni msaada wa kufaa ili kuzuia matokeo ya kuangamiza ya matata ya nyakati zetu.
 
«Tazama, mama yako! » (Yoh 19:27)
 
7. Dalili mbalimbali zinaonyesha jinsi Bikira mtakatifu anavyotaka kutekeleza leo pia, hasa kwa njia ya sala hiyo, juhudi za kimama ambazo Mkombozi alipokuwa mahututi alizikabidhi wana wote wa Kanisa katika nafsi ya mwanafunzi mpendwa:  "Mama tazama mwanao" (Yoh 19:26). Zinajulikana nafasi mbalimbali ambazo Mama wa Kristo, katika karne ya XIX na XX alijitokeza na kusema ili kuhimiza taifa la Mungu kutumia aina hiyo ya sala ya kuzama katika mafumbo.
Kwa namna ya pekee napenda kukumbusha maono ya Lurdi na Fatima, kutokana na jinsi yalivyoathiri mpaka leo maisha ya Wakristo na kuthibitishwa rasmi na Kanisa; patakatifu hapo pawili ni shabaha za wahiji wengi wanaojitafutia faraja na tumaini.
 

Kwenye nyayo za mashahidi

 
8. Haiwezekani kutaja umati usiohesabika wa watakatifu walioiona katika Rozari njia halisi ya utakatifu. Inatosha kukumbuka mtakatifu Alois Maria Grignion de Montfort, mwandishi wa kitabu azizi kuhusu Rozari, na karibu nasi zaidi, padri Pio wa Pietrelcina, ambaye hivi karibuni nimefurahi kumtangaza kuwa ni mtakatifu.
Halafu karama maalumu ya kuwa mtume halisi wa Rozari alikuwa nayo mwenye heri Bartolo Longo. Safari yake ndefu ya utakatifu ilitegemea mnong'ono aliousikia kilindini mwa moyo wake: "Anayeeneza Rozari ataokoka!" Juu ya msingi huo alijisikia kuitwa ajenge huko Pompei kanisa kwa heshima ya Bikira wa Rozari takatifu katika mandhari ya mji wa zamani ambao ulifikiwa tu na ujumbe wa Kikristo kabla haujateketezwa na mlipuko wa volkeno Vesuvio mwaka 79,  na ambao karne nyingi baadaye ulielea tena kutoka majivu yake kama ushuhuda wa mianga na vivuli vya ustaarabu wa zamani.
Kwa kazi yake yote, na hasa kwa "Sabato Kumi na Tano", Bartolo Longo alistawisha kiini cha Kikristo na cha kuzama katika mafumbo cha Rozari, akitiwa moyo na kutegemezwa kwa namna ya pekee na Leo XIII, « Papa wa Rozari ».
 
 
 

 

 

SURA YA KWANZA

 
KUMKAZIA MACHO KRISTO PAMOJA NA MARIA
 
 
 

Uso mwangavu kama jua

 
9. "Aligeuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua" (Math 17:2). Ukurasa wa Injili wa Kristo kugeuka sura, ambapo mitume watatu Petro, Yakobo na Yohane wanaonekana kama wamechanganyikiwa na uzuri wa Mkombozi, unaweza kuchukuliwa kama picha ya sala hasa ya Kikristo. Kuukazia macho uso wa Kristo, kutambua fumbo lake katika safari ya kawaida na ya uchungu ya ubinadamu wake, hadi kuhisi uangavu wa Kimungu uliodhihirika moja kwa moja katika Mfufuka aliyetukuzwa kuumeni kwa Baba, ndiyo kazi ya kila mfuasi wa Kristo; kwa hiyo ni kazi yetu pia. Tukiukazia macho uso huo tunajiweka tayari tuupokee fumbo la uzima wa Utatu mtakatifu, ili kung'amua kwa namna mpya daima upendo wa Baba na kujaa furaha ya Roho Mtakatifu. Hapo linatimia kwetu pia neno la mtume Paulo: "Tukiurudisha utukufu wa Bwana, kama vile katika kioo, tunabadilishwa tufanane na mfano uo huo, toka utukufu hata utukufu, kama vile kwa utukufu utokao kwa Bwana, aliye Roho" (2Kor 3:18).
 

Maria kielelezo cha sala hasa

 
10. Maria ni kielelezo bora cha kumkazia macho Kristo. Sura ya Mwana ni ya kwake kwa namna ya pekee. Alitungwa tumboni mwake, akichukua toka kwake sura ya kufanana naye kibinadamu ambayo inadokeza ujirani wa Kiroho ambao kwa hakika ni mkubwa zaidi. Hakuna aliyejitolea kuukazia macho uso wa Kristo kuliko alivyofanya Maria. Kwa namna fulani macho ya moyo wake yalianza kumuelekea tangu apashwe habari, alipomchukua mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu; miezi iliyofuata alianza kuhisi uwemo wake tumboni na kutabiri sura yake. Hatimaye alipomzaa Bethlehemu macho ya mwili wake pia yaliuelekea kwa hisani uso wa Mwana, huku akimvika nguo za kitoto na kumlaza horini (taz. Lk 2:7).
Tangu hapo mtazamo wake, uliojaa daima mshangao wa kiibada, haukubandukana naye tena. Pengine ukawa mtazamo wa kuuliza swali, kama vile katika tukio la Yesu kupotea hekaluni: «Mwanangu, mbona umetutenda hivi?» (Lk 2:48); kwa vyovyote ukawa mtazamo wa kupenya, unaoweza kusoma moyoni mwa Yesu, hata kuhisi miguso iliyofichika na kutabiri machaguo yake, kama alivyofanya Kana (taz. Yoh 2:5); mara nyingine ukawa mtazamo wenye uchungu, hasa chini ya msalaba ambapo ukawa tena, kwa namna fulani, mtazamo wa 'mwanamke anayejifungua', kwa kuwa Maria hakushiriki tu mateso na kifo cha Mwana pekee, bali alimpokea mtoto mpya aliyekabidhiwa katika mwanafunzi mpendwa (taz. Yoh 19:26-27); asubuhi ya Pasaka ukawa mtazamo mwangavu kwa furaha ya ufufuko na hatimaye ukawa mtazamo motomoto kwa ajili ya Roho kumiminwa siku ya Pentekoste (taz. Mdo 1:14).
 

Kumbukumbu za Maria

 
11. Maria aliishi macho kwa Kristo na kutia maanani kila neno lake: «Aliyaweka maneno hayo yote, akiyafikiri moyoni mwake» (Lk 2:19; taz. 2:51). Kumbukumbu za Yesu, zilizochapika rohoni mwake, zilimfuata katika nafasi yoyote, zikimfanya arudie kimawazo matukio mbalimbali ya maisha yake karibu na Mwana. Kumbukumbu hizo ndizo zilizounda, kwa namna fulani, 'rozari' ambayo mwenyewe alisali mfululizo siku zote za maisha yake duniani.
Pia sasa, kati ya nyimbo za furaha za Yerusalemu wa mbinguni, sababu zake za kushukuru na kusifu zinabaki zilezile. Ndizo zinazomuelekeza kulishughulikia kimama Kanisa linalohiji, ambapo mwenyewe anaendelea kutekeleza tangazo lake kama mwenezainjili. Maria anawapendekezea mfululizo waamini 'mafumbo' ya Mwanae, akitamani yatazamwe yaweze kueneza uwezo wote wa kuokoa uliyo nayo. Jumuia ya Kikristo inaposali Rozari inajilinganisha na kumbukumbu na mtazamo wa Maria.
 

Rozari, sala ya kuzamia mafumbo ya imani

 
12. Rozari, kuanzia mang'amuzi yenyewe ya Maria, ni sala hasa ya kuzamia mafumbo ya imani. Ingekosa sura hiyo isingekuwa yenyewe tena, kama alivyosisitiza Paulo VI: «Pasipo kuzama katika mafumbo, Rozari ni kama mwili usio na roho, na inaingia hatari ya kukariri maneno kimashine tu na hivyo kupinga onyo la Yesu: 'Mkiwa katika kusali, msipayukepayuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi' (Math. 6:7). Kwa maumbile yake, sala ya Rozari inadai mwendo mtulivu na kama kusimama kwa kuwaza, ambavyo vimsaidie anayesali atafakari mafumbo ya maisha ya Bwana, ambayo yatazamwe kupitia moyo wa Mama yule aliyekuwa karibu zaidi na Bwana, na vifunue utajiri wake usiopimika».
Inafaa tuzingatie wazo hilo la dhati la Paulo VI, ili kutokeza sura mbalimbali za Rozari ambazo zinatia maanani sifa yake ya kuwa sala ya kumkazia macho Kristo.
 

Kumkumbuka Kristo pamoja na Maria

 
13. Kwa Maria, kuzama katika mafumbo ni hasa kukumbuka. Lakini ni lazima tuelewe hilo kwa maana ya Kibiblia ya neno (zakar), ambayo inafanya matendo aliyoyatenda Mungu katika historia ya wokovu yawe ya leo. Biblia ni simulizi la matukio ya wokovu, ambayo kilele chake ni Kristo mwenyewe. Matukio hayo siyo "jana" tu, bali ni "leo" ya wokovu. Jambo hilo la kufanya tukio lililopita liwe la leo pia linatendeka hasa katika liturujia: yale ambayo Mungu aliyatenda karne kadhaa zilizopita hayawahusu tu wale walioyashuhudia kwa wakati wake, bali yanamfikia kwa zawadi yake ya neema mtu wa wakati wowote. Kwa namna fulani hilo ni kweli pia kwa njia nyingine za kujihusisha kwa imani na matukio hayo: «kuyakumbuka» kwa msimamo wa imani na upendo, maana yake ni kujiweka wazi kupokea neema ambayo Kristo ametupatia kwa mafumbo ya maisha, kifo na ufufuko wake.
Kwa hiyo, wakati ni lazima tusisitize tena pamoja na Mtaguso wa pili wa Vatikano kwamba liturujia, iliyo utekelezaji wa ukuhani wa Kristo na ibada rasmi ya hadhara, ndiyo «kilele ambacho utendaji wote wa Kanisa unakilenga na papo hapo chemchemi ambamo nguvu zake zote zinabubujika», ni lazima pia tukumbuke kwamba maisha ya Kiroho «hayaishii katika kushiriki liturujia takatifu tu. Mkristo ameitwa kusali pamoja na wenzake, hata hivyo anatakiwa pia kuingia katika chumba chake cha ndani ili kumuomba Baba sirini (taz. Mt 6:6); tena anatakiwa kusali bila ya kikomo, kama mtume Paulo alivyofundisha (taz. 1Ts 5:17)». Rozari inaingia kwa namna yake maalumu  katika mandhari hiyo yote ya sala 'isiyokoma', na ikiwa liturujia, iliyo kazi ya Kristo na ya Kanisa lake, ni kazi ya wokovu kwa namna bora, Rozari, iliyo tafakuri juu ya Kristo pamoja na Maria, ni kuzama ndani ya mafumbo kunakoleta wokovu. Kwa kuwa kuzama katika maisha ya Mkombozi, fumbo baada ya fumbo, kunasababisha kwamba, yale ambayo mwenyewe aliyatenda na ambayo liturujia inafanya yawe ya leo, yapokewe na mwamini kwa dhati na kuunda maisha yake.

 

Kufundishwa na Maria juu ya Kristo

 
14. Kristo ndiye Mwalimu hasa, yeye aliye mfunuaji na ufunuo wenyewe. Si swala la kujifunza tu maneno aliyoyafundisha, bali la 'kumsoma mwenyewe'. Lakini nani mwalimu mzoefu kuliko Maria katika jambo hilo? Ikiwa upande wa Mungu Roho Mtakatifu ndiye Mwalimu wa ndani anayetufikisha kwenye ukweli wote wa Kristo (taz. Yoh 14:26; 15:26; 16:13), upande wa binadamu hakuna anayemfahamu Kristo vizuri kuliko Maria, hakuna anayeweza kama Mama yake kutuingiza katika ujuzi wa dhati wa fumbo lake.
'Ishara' ya kwanza iliyotendwa na Yesu - kugeuza maji kuwa divai kwenye arusi ya Kana - inatuonyesha Maria katika nafasi hiyo ya mwalimu, akiwahimiza watumishi watekeleze maagizo ya Kristo (taz. Yoh 2:5). Na tunaweza kubuni kwa hakika kwamba, kazi hiyo mwenyewe aliifanya kwa ajili ya wanafunzi baada ya Yesu kupaa mbinguni, ambao alibaki pamoja nao wakimngojea Roho Mtakatifu, akawafariji katika mwanzo wa utume wao. Kupitia pamoja na Maria mafumbo ya Rozari ni kama kuketi 'shuleni' pa Maria ili kumsoma Kristo, ili kupenya siri zake, ili kuelewa ujumbe wake. Shule hiyo ya Maria inaleta faida kubwa, hasa tukizingatia kwamba anafanya kazi hiyo kwa kutupatia kwa wingi vipaji vya Roho Mtakatifu na papo hapo kwa kutupendekezea mfano wa ile «hija ya imani», ambayo yeye ni mwalimu wake asiye na kifani. Mbele ya kila fumbo la Mwanae, mwenyewe anatualika, kama alivyofanya siku aliyopashwa habari na malaika, tuulize kwa unyenyekevu maswali yanayotufungulia mwanga, halafu tumalizie daima kwa utiifu wa imani: «Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema» (Lk 1:38).
 

Kujilinganisha na Kristo pamoja na Maria

 
15. Maisha ya Kiroho ya Kikristo sifa yake kuu ni juhudi ya mwanafunzi kujilinganisha na Mwalimu wake zaidi na zaidi (taz. Rom 8:29; Fil 3:10,21). Miminiko la Roho katika ubatizo, linalomwingiza mwamini kama tawi ndani ya mzabibu ambao ni Kristo (taz. Yoh 15:5), linamfanya kiungo cha mwili wake wa fumbo (taz. 1Kor 12:12; Rom 12:5). Lakini umoja huo wa msingi unatakiwa kufuatwa na safari ya kuungana naye zaidi na zaidi, ambayo ielekeze zaidi na zaidi mwenendo wa mwanafunzi kadiri ya 'nia' ya Kristo: «Iweni na nia iyohiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu » (Fil 2:5). Kadiri ya maneno ya Mtume ni lazima «kumvaa Kristo» (taz. Rom 13:14; Gal 3:27).
Katika safari ya Kiroho ya Rozari, ambayo msingi wake ni kuukazia macho mfululizo uso wa Kristo pamoja na Maria, kipeo hicho kigumu cha kujilinganisha naye kinalengwa kwa njia ya kumkaribia 'kirafiki'. Hiyo inatuingiza kwa urahisi katika maisha ya Kristo na kutufanya 'tupumue' hisia zake. Kuhusu jambo hilo mwenye heri Bartolo Longo alisema, «Kama vile marafiki wawili, wakishirikiana mara nyingi, huwa wanafanana katika mwenendo pia, sisi tukiongea kidugu na Yesu na Bikira, katika kutafakari mafumbo ya Rozari, na kuishi pamoja nao kwa Ekaristi, tunaweza kufanana nao, kadiri unyonge wetu unavyoruhusu, na kujifunza kutoka kwa vielelezo hivyo bora maisha ya unyenyekevu, ya ufukara, yaliyofichika, ya subira na makamilifu».
Kwa safari hiyo ya kujilinganisha na Kristo, katika Rozari tunajiaminisha kwa namna ya pekee kwa kazi ya kimama ya Bikira mtakatifu. Yeye aliye mzazi wa Kristo, huku akiwa  mwenyewe kiungo cha Kanisa, tena «kiungo bora na cha pekee kabisa», kwa wakati huohuo ni pia 'Mama wa Kanisa'. Kulingana na hadhi hiyo anazidi 'kuzaa' wana kwa Mwili wa fumbo wa Mwanae. Anafanya hivyo kwa njia ya dua, akiwaombea miminiko la Roho ambalo halina mwisho. Maria ndiye picha kamili ya umama wa Kanisa.
Rozari inatusogeza kifumbo karibu na Maria aliyewajibika kusaidia ustawi wa kibinadamu wa Kristo katika nyumba ya Nazareti. Hiyo inamwezesha kutulea na kutuunda kwa juhudi hizohizo hadi Kristo “aundwe” kikamilifu ndani mwetu (taz. Gal 4:19). Kazi hiyo ya Maria, ambayo inategemea na kulenga kabisa ile ya Kristo, “haizuii hata kidogo muungano wa moja kwa moja wa waamini na Kristo, bali inausaidia”. Ndilo wazo angavu lililotokezwa na Mtaguso wa pili wa Vatikano, ambalo nimeling'amua kwa nguvu sana maishani mwangu, nikilifanya msingi wa tamko langu la kiaskofu: Totus tuus. Inavyoeleweka, tamko hilo linatokana na mafundisho ya mtakatifu Alois Maria Grignion de Montfort, ambaye alieleza ifuatavyo nafasi ya Maria katika safari ya kila mmojawetu ya kujilinganisha na Kristo: «Ukamilifu wetu wote umo katika kulingana, kuungana na kuwekwa wakfu kwa Yesu Kristo. Kwa hiyo bila ya shaka ibada iliyo kamili kuliko zote ni ile ambayo inatulinganisha, inatuunganisha na kutuweka wakfu kikamilifu zaidi kwa Yesu Kristo. Basi, kwa kuwa Maria ndiye kiumbe aliyelingana zaidi na Yesu Kristo, kati ya ibada zote ile inayomweka wakfu na kumlinganisha zaidi mtu kwa Bwana wetu ni ibada kwa Maria, Mama yake mtakatifu, tena kadiri atakavyowekwa wakfu kwake atawekwa wakfu kwa Yesu Kristo». Hakuna nafasi nyingine kuliko Rozari ambapo njia ya Kristo na ya Maria zinaonekana kuwa ni moja kwa dhati. Maria anaishi ndani ya Kristo tu na kwa ajili ya Kristo!
 

Kumuomba Kristo pamoja na Maria

 
16. Kristo ametualika tumuelekee Mungu kwa udumifu na tumaini ili tusikilizwe: «Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa» (Math 7:7). Msingi wa uwezo huo wa sala ni wema wa Baba, lakini pia ushenga wa Kristo mwenyewe mbele yake (taz. 1Yoh 2:1) na kazi ya Roho Mtakatifu ambaye «hutuombea» kadiri ya mipango ya Mungu (taz. Rom 8:26-27). «Kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo» (Rom 8:26) na pengine hatusikilizwi kwa sababu «tunaomba vibaya» (taz. Yak 4:2-3).
Ili kuchangia sala ambayo Kristo na Roho wanabubujisha moyoni mwetu, Maria anaingia kati kwa maombezi yake ya kimama. «Sala ya Kanisa ni kama inategemezwa na sala ya Maria». Kwa kweli, Yesu, mshenga pekee, akiwa ndiye njia ya sala yetu, Maria, aliye picha yake angavu, anaionyesha hiyo njia na «kwa msingi wa ushirikiano huo wa pekee wa Maria na kazi ya Roho Mtakatifu, Makanisa yamestawisha sala kwa Mama mtakatifu wa Mungu, yakifanya ilenge kwenye nafsi ya Kristo iliyodhihirishwa katika mafumbo yake». Kwenye arusi ya Kana Injili inaonyesha hiyo nguvu ya maombezi ya Maria, aliyejifanya sauti ya shida za watu kwa Yesu: «Hawana divai» (Yoh 2:3).
Rozari ni tafakuri na dua kwa pamoja. Kumlilia kwa bidii Mama wa Mungu, msingi wake ni tumaini la kwamba maombezi yake ya kimama yanaweza yote moyoni mwa Mwanae. Alivyosema mwenye heri Bartolo Longo katika Dua kwa Bikira, akitumia neno la kusisimua linalohitaji kueleweka vizuri, Maria ni «Mwenyezi kwa neema». Hakika hiyo, ambayo chanzo chake ni Injili, imeimarishwa na mang'amuzi ya taifa la Kristo. Mwanashairi bora Dante aliitafsiri vizuri ajabu, kufuatana na mtakatifu  Bernardo, akiimba: «Mama, wewe u mkuu na mwenye uwezo hivi kwamba, /  anayetaka neema asikukimbilie wewe, / hamu yake inataka kuruka pasipo mabawa». Maria, patakatifu pa Roho Mtakatifu (taz. Lk 1:35), wakati anapoombwa nasi katika Rozari, anatusimamia mbele ya Baba aliyemjaza neema na ya Mwana aliyezaliwa kutoka tumboni mwake, akisali pamoja nasi na kwa ajili yetu.
 
Kumtangaza Kristo pamoja na Maria
 
17. Rozari ni pia safari ya kutangaza na kuchimba, ambamo fumbo la Kristo linatokezwa upya mfululizo kwa ngazi mbalimbali za maisha ya Kikristo. Namna yake ni ya kulitokeza upande wa sala na wa kuzama ndani ya mafumbo, ambayo inalenga kumuunda mfuasi kadiri ya moyo wa Kristo. Kwa kweli katika kusali Rozari, ikiwa sehemu zake zote zinazoweza kuchangia tafakuri ya nguvu zinatumika ipasavyo, inapatikana nafasi muhimu ya katekesi, hasa katika adhimisho la kijumuia kwenye parokia na patakatifu. Wachungaji wanatakiwa kuitumia nafasi hiyo. Bikira wa Rozari anaendelea hivyo pia kazi yake ya kumtangaza Kristo. Historia ya Rozari inaonyesha jinsi sala hiyo ilivyotumiwa hasa na Wadominiko, katika kipindi kilichokuwa kigumu kwa Kanisa kutokana na uenezi wa uzushi. Leo tuko mbele ya changamoto mpya. Kwa nini tusishike tena tasbihi mikononi kwa imani ile waliyokuwa nayo waliotutangulia? Rozari inadumu kuwa na nguvu zake zote na kuendelea kuwa silaha muhimu kati ya vifaa vya kichungaji vya kila mwenezainjili halisi. 
 
 
 
 
SURA YA PILI
 
MAFUMBO YA KRISTO - MAFUMBO YA MAMA
 
 
 

Rozari «muhtasari wa Injili»

 
18. Hatuwezi kuanza kuukazia macho uso wa Kristo bila ya kusikiliza, katika Roho, sauti ya Baba, kwa sababu «hakuna amjuaye Mwana, ila Baba» (Math 11:27). Karibu na Kaisarea Filipi, baada ya ungamo la Petro, Yesu alifafanua asili ya hisi hiyo sahihi hivi ya undani wake mwenyewe: «Mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni» (Math 16:17). Kwa hiyo ni lazima kufunuliwa kutoka juu. Lakini ili tuupokee ufunuo huo ni lazima kusikiliza. Mang'amuzi ya kimya na ya sala tu yanatupatia upeo wa kufaa ambapo unaweza kukomaa na kustawi ujuzi halisi zaidi wa fumbo hilo, ambao unaunganisha na kutia uaminifu.
Rozari ni njia mojawapo ya mapokeo ya sala ya Kikristo kwa ajili ya kuzama katika uso wa Kristo. Papa Paulo VI aliifafanua hivi: « Rozari ikiwa sala ya Kiinjili, ambayo kiini chake ni fumbo la umwilisho ulioleta ukombozi, basi ni sala inayomlenga Kristo moja kwa moja. Kwa kuwa hata jambo lake maalumu zaidi  - yaani kukariri kilitania Salamu Maria - linakuwa sifa isiyokoma kwa Kristo, lengo kuu la tangazo la malaika na la salamu ya mama wa Mbatizaji: 'Mzao wa tumbo lako amebarikiwa' (Lk 1:42). Tuseme zaidi: kukariri Salamu Maria ni kama kitambaa ambacho juu yake tunafuma tendo la kuzama katika mafumbo: Yesu anayekumbushwa na kila Salamu Maria ni yuleyule ambaye mfululizo wa mafumbo unatutolea mara kwa mara kama Mwana wa Mungu na wa Bikira».
 

Ukamilisho wa kufaa

 
19. Kati ya mafumbo mengi ya maisha ya Kristo, Rozari, kwa jinsi ilivyoundika katika desturi iliyopitishwa na mamlaka ya Kanisa, inayapendekeza machache tu. Chaguo hilo lililazimishwa na mpango asili wa sala hiyo wa kulingana na idadi ya Zaburi 150.
Hata hivyo naona kwamba, ili kuongeza uzito wa Kikristo wa Rozari, inafaa kuikamilisha kwa namna ambayo, ingawa inaachwa ifanyiwe kazi kwa hiari na mtu mmojammoja na jumuia nzima, iiwezeshe kukumbatia pia matendo ya maisha ya hadhara ya Kristo kati ya ubatizo na mateso. Kwa kuwa katikati ya mafumbo hayo tunakazia macho pande muhimu za nafsi ya Kristo kama yule aliyetufunulia Mungu moja kwa moja. Ndiye yule ambaye, kisha kutambulishwa kama Mwana mpendwa wa Baba kwenye ubatizo katika mto Yordani, aliutangaza ujio wa Ufalme, aliushuhudia kwa matendo na kutangaza madai yake. Ni katika miaka ya maisha ya hadhara kwamba  fumbo la Kristo lilidhihirika kwa namna ya pekee kama fumbo la mwanga: «Muda nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu» (Yoh 9:5).
Basi, ili Rozari iweze kuitwa kwa haki zaidi 'muhtasari wa Injili', inafaa kwamba, kisha kukumbuka umwilisho na maisha yaliyofichika ya Kristo (mafumbo ya furaha), na kabla ya kuzingatia uchungu wa mateso (mafumbo ya uchungu) na ushindi wa ufufuko (mafumbo ya utukufu), tafakuri ilenge pia nafasi kadhaa za maana zaidi za maisha ya hadhara (mafumbo ya mwanga). Ongezeko hilo la mafumbo mapya, bila ya kuhatarisha jambo lolote la msingi katika sura ya kimapokeo ya sala hiyo, linakusudiwa kuifanya izingatiwe upya katika maisha ya Kiroho ya Wakristo, kama namna halisi ya kuingizwa vilindini mwa moyo wa Kristo, ulio kina kirefu cha furaha na mwanga, uchungu na utukufu.
 
Mafumbo ya furaha
 
20. Mfululizo wa kwanza, ule wa 'mafumbo ya furaha', kwa kweli  sifa yake maalumu ndiyo furaha iliyosambazwa na tukio la umwilisho. Hiyo ni wazi tangu Kupasha Habari, ambapo salamu ya Gabrieli kwa Bikira wa Nazareti inajilinganisha na mwaliko wa kuwa na furaha ya Kimasiha: «Furahi, Maria». Tangazo hilo ni lengo la historia yote ya wokovu, tena la historia ya ulimwengu pia. Kwa sababu, ikiwa mpango wa Baba ni kujumlisha vyote katika Kristo (taz. Ef 1:10), kwa namna fulani ulimwengu wote ndio uliofikiwa na fadhili ya Kimungu ambayo Baba alimuinamia Maria ili kumfanya Mama wa Mwanae. Upande mwingine, binadamu wote ni kama wanaingia ndani ya fiat ambayo Maria aliyakubali mara matakwa ya Mungu.
Halafu tukio la kukutana na Elizabeti limejaa shangwe, ambapo sauti yenyewe ya Maria na uwemo wa Kristo tumboni mwake vilifanya Yohane «kikaruka kwa shangwe» (taz. Lk 1:44). Limejaa furaha vilevile tukio la Bethlehemu, ambapo kuzaliwa kwa Mtoto wa Kimungu, Mwokozi wa dunia, kuliimbwa na malaika na kutangazwa kwa wachungaji kama «furaha kuu» (Lk 2:10).
Lakini mafumbo mawili ya mwisho, ingawa yanaendelea kuwa na ladha ya furaha, yanadokeza tayari dalili za janga. Kwa kuwa Kutolewa hekaluni, huku kukitokeza furaha ya kuwekwa wakfu na ya kumzamisha mzee Simeoni katika fumbo, kunaleta pia utabiri juu ya «ishara itakayonenewa» ambayo huyo Mtoto atakuwa kwa Israeli, na juu ya upanga utakaochoma moyo wa Mama (taz. Lk 2:34-35). Vilevile ni la furaha na la kusikitisha kwa pamoja tukio la Yesu hekaluni akiwa na umri wa miaka kumi na miwili. Hapo alitokea katika hekima yake ya Kimungu, huku akisikiliza na kuhoji, akiwa kimsingi yule mwenye 'kufundisha'. Ufunuo wa fumbo lake kama Mwana anayewajibika kabisa kwa mambo ya Baba ni tangazo la ile nia imara ya Kiinjili ambayo mbele ya madai ya moja kwa moja ya Ufalme inatia shakani hata mafungamano mapendevu zaidi kwa binadamu. Yosefu na Maria wenyewe, waliohangaika na kufadhaika, «hawakuelewa na neno hilo alilowaambia» (Lk 2:50).
Hivyo kutafakari mafumbo 'ya furaha' ni kuingia ndani ya sababu kuu na maana ya dhati ya furaha ya Kikristo. Ni kukazia macho uhalisi wa fumbo la umwilisho na utabiri usio wazi wa fumbo la uchungu wenye kuokoa. Maria anatuongoza tuelewe siri ya furaha ya Kikristo, akitukumbusha kwamba Ukristo ni hasa euangelion, 'habari njema', ambayo kiini chake, tena yaliyomo yake yote ni nafsi ya Kristo, Neno aliyefanyika mwili, Mwokozi pekee wa ulimwengu.
 

Mafumbo ya mwanga

 
21. Sala hasa, ikivuka toka utoto na maisha ya Nazareti hadi maisha ya hadhara ya Yesu, inatufikisha kwenye mafumbo ambayo yanaweza kuitwa kwa namna ya pekee 'mafumbo ya mwanga'. Kwa kweli, fumbo lote la Kristo ni mwanga. Ndiye «nuru ya ulimwengu» (Yoh 8:12). Lakini sifa hiyo inajitokeza hasa katika miaka ya maisha ya hadhara, ambapo yeye alitangaza habari njema ya Ufalme. Nikitaka kuionyesha jumuia ya Kikristo nafasi tano za maana - mafumbo 'ya mwanga' – za kipindi hicho cha maisha ya Kristo, naona inafaa kuzibainisha kama ifuatavyo: 1. katika ubatizo wake kwenye Yordani, 2. katika kujifunua kwake kwenye arusi ya Kana, 3. katika kutangaza Ufalme wa Mungu pamoja na mwaliko wa kuongoka, 4. katika kung’aa kwake alipogeuka sura, na, hatimaye, 5. katika kuweka ekaristi, sakramenti ya fumbo la Pasaka.
Kati ya mafumbo hayo kila mojawapo linafunua Ufalme uliokwishafika katika nafsi yenyewe ya Yesu. Kwanza, ubatizo kwenye Yordani. Hapo, Kristo aliposhukia maji ya mto, kama yule asiye na doa anayejifanya ‘dhambi’ kwa ajili yetu (taz. 2Kor 5:21), mbingu zilifunguka na sauti ya Baba ilimtangaza kuwa ni Mwanae mpenzi (taz. Math 3:17 na aya sambamba), huku Roho akimshukia ili kumweka wakfu kwa utume unaomkabili. Pili, mwanzo wa ishara huko Kana (taz. Yoh 2:1-12), ambapo Kristo, akigeuza maji kuwa divai, aliifungua mioyo ya wanafunzi isadiki kutokana na Maria kuingilia kati, yeye aliye wa kwanza kati ya waamini. Tatu, mahubiri ambayo Yesu alitangaza ujio wa Ufalme wa Mungu na kualika watu watubu (taz. Mk 1:15), akiondolea dhambi za wanaomkaribia kwa tumaini nyenyekevu (taz. Mk 2:3-13; Lk 7:47-48), mwanzo wa ile huduma ya huruma atakayoendelea kutoa hadi mwisho wa dunia, hasa kwa njia ya sakramenti ya upatanisho aliyolikabidhi Kanisa lake (taz. Yoh 20:22-23). Halafu kwa namna ya pekee tukio la kugeuka sura, ambalo kadiri ya mapokeo lilitokea juu ya mlima Tabori. Utukufu wa umungu uling’aa katika uso wa Kristo, huku Baba akimtambulisha kwa mitume waliochanganyikiwa na uzuri huo akidai wamsikilize (taz. Lk 9:35 na aya sambamba) na wajiandae kuishi pamoja naye nafasi chungu ya mateso, ili kufikia pamoja naye furaha ya ufufuko na maisha yaliyogeuzwa sura na Roho Mtakatifu. Hatimaye, ni fumbo la mwanga tendo la kuweka ekaristi, ambamo Kristo anajifanya chakula kwa Mwili wake na Damu yake ndani ya maumbo ya mkate na divai, akishuhudia «upeo» wa upendo wake kwa ajili ya ulimwengu (Yoh 13:1), ambao akajitoa sadaka kwa wokovu wake.
Uwepo wa Maria hauonekani katika mafumbo hayo, isipokuwa Kana. Injili zinadokeza tu mara moja moja uwepo wake katika nafasi hii au hii ya mahubiri ya Yesu (taz. Mk 3:31-35; Yoh 2:12) na hazisemi kitu kuhusu uwezekano wa kuwepo kwake karamuni wakati wa kuweka ekaristi. Lakini kazi aliyoifanya Kana inasindikiza, kwa namna fulani, safari yote ya Kristo. Ufunuo ule ambao katika ubatizo kwenye Yordani ulitolewa na Baba moja kwa moja ukarudiwa na Mbatizaji kama mwangwi wake, huko Kana ulikuwemo kinywani mwa Maria, ulipogeuka kuwa onyo kuu la kimama ambalo analitoa kwa Kanisa la nyakati zote: «Lolote atakalowaambia, fanyeni» (Yoh 2:5). Hilo ni onyo linalofaa kutangulia maneno na ishara ya Kristo katika maisha ya hadhara, likiendelea kuonekana nyuma ya 'mafumbo yote ya mwanga' ili tuyazingatie kadiri ya Maria.
 

Mafumbo ya uchungu

 
22. Injili zinatia maanani sana mafumbo ya uchungu ya Kristo. Tangu zamani ibada ya Kikristo, hasa wakati wa Kwaresima, kupitia Njia ya Msalaba, imezingatia kwa makini kila tukio la mateso, ikihisi kwamba humo ndimo kilele cha ufunuo wa upendo na ndimo chemchemi ya wokovu wetu. Rozari imechagua baadhi ya matukio ya mateso, ikimhimiza anayeisali kuyakazia macho ya moyo na kuyaishi upya. Safari ya tafakuri inaanza huko Getsemani, ambako Kristo aliishi nafasi ya uchungu wa pekee mbele ya matakwa ya Baba, ambayo udhaifu wa mwili unashawishiwa kuyakaidi. Huko Kristo alishika nafasi ya vishawishi vyote vya binadamu, na mbele ya dhambi zote za binadamu, ili amuambie Baba: «Si mapenzi yangu, bali yako yatendeke» (Lk 22:42 na aya sambamba). ‘Ndiyo’ yake hiyo ilipindua 'hapana' ya wazazi wetu wa kwanza bustanini mwa Edeni. Jinsi utiifu huo kwa matakwa ya Baba ulivyokuwa mgumu kwake inajitokeza katika mafumbo yanayofuata ya kupanda hadi Kalivari, kupigwa mijeledi, kutiwa taji la miba, kufa msalabani, ambapo alidhalilishwa kupita kiasi: Ecce homo!
Katika kudhalilishwa hivyo haufunuliwi tu upendo wa Mungu, bali pia maana yenyewe ya binadamu. Ecce homo: anayetaka kufahamu mtu alivyo, anapaswa kutambua maana, mzizi na utimilifu wake katika Kristo, Mungu aliyejishusha kwa upendo «hata mauti, naam, mauti ya msalaba» (Fil 2:8). Mafumbo ya uchungu yanamuongoza mwamini kuishi upya kifo cha Yesu kwa kujiweka chini ya msalaba karibu na Maria, ili kuzama pamoja na Mama katika kilindi cha upendo wa Mungu kwa binadamu na kuhisi nguvu zake zote za kuletea uhai mpya.

Mafumbo ya utukufu

 
23. «Kuukazia macho uso wa Kristo hakuwezi kuishia kwenye picha yake kama msulubiwa. Yeye yupo amefufuka!». Tangu zamani Rozari inatokeza hakika hiyo ya imani, ikimualika mwamini avuke ng’ambo ya giza la mateso, ili kuukazia macho utukufu wa Kristo katika ufufuko na katika Kupaa mbinguni. Mkristo akimkazia macho Mfufuka anavumbua upya sababu za imani yake (taz. 1Kor 15:14), na kuishi upya furaha sio tu ya wale ambao Kristo aliwatokea – mitume, Magdalena, wanafunzi wa Emau -, bali pia furaha ya Maria, ambaye alitakiwa kuwa na mang’amuzi si mapungufu ya uhai mpya wa Mwana aliyetukuzwa. Katika utukufu huo ambao, kwa Kupaa kwake, ulimweka Kristo kuumeni kwa Baba, Maria mwenyewe akainuliwa kwa Kupalizwa kwake, akifikia, kwa fadhili ya pekee kabisa, kutanguliza hali waliyoandaliwa waadilifu wote kwa ufufuko wa mwili. Hatimaye, akitiwa taji la utukufu – anavyoonekana katika fumbo la mwisho la utukufu – anang’aa kama Malkia wa malaika na wa watakatifu, utangulizi na kilele cha hali ya milele ya Kanisa.
Kama kiini cha safari hiyo ya utukufu wa Mwana na wa Mama, Rozari inaipanga, katika fumbo la tatu la utukufu, Pentekoste, inayoonyesha uso wa Kanisa kama familia iliyounganika na Maria, iliyouhishwa na miminiko la nguvu la Roho, iliyo tayari kwa utume wa uinjilishaji. Kuzama katika fumbo hilo, sawa na mafumbo mengine ya utukufu, kunatakiwa kuwafanya waamini waelewe kwa namna hai zaidi na zaidi maisha yao mapya katika Kristo, ndani ya ukweli wa Kanisa, maisha ambayo tukio la Pentekoste ndiyo ‘picha' yake bora. Hivyo mafumbo ya utukufu yanalisha ndani ya waamini tumaini la lengo la milele wanalolielekea kama viungo vya taifa la Mungu linalohiji katika historia. Hiyo inatakiwa kuwasukuma washuhudie kishujaa ile «habari njema» inayotia maanani maisha yao yote.
 

Toka 'mafumbo' hadi 'fumbo': njia ya Maria

 
24. Bila ya shaka hiyo mifululizo ya tafakuri inayopendekezwa na Rozari takatifu haimalizi yote, ila inakumbusha yaliyo ya lazima, ikiingiza roho ionje ule ujuzi wa Kristo ambao unachota mfululizo kwenye chemchemi safi ya kitabu cha Injili. Kila jambo la maisha ya Kristo, linavyosimuliwa na Wainjili, linang’aa kwa fumbo lile lipitalo ujuzi wote (taz. Ef 3:19).  Ndilo fumbo la Neno aliyefanyika mwili, ambamo «unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili» (Kol 2:9). Ndiyo sababu Katekisimu ya Kanisa Katoliki inasisitiza sana mafumbo ya Kristo, ikikumbusha kwamba «katima maisha ya Yesu yote ni ishara ya fumbo lake». Neno la «duc in altum» la Kanisa katika milenia ya tatu linapimwa na uwezo wa Wakristo wa «kujua kabisa siri ya Mungu, yaani, Kristo; ambaye ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika» (Kol 2:2-3). Matashi motomoto ya barua kwa Waefeso (3:17-19)  yanaelekea kila aliyebatizwa: «Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate [...] kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu».
Rozari inataka kutumikia kipeo hicho, ikitolea 'siri' ya kujiweka wazi kwa urahisi zaidi kumjua Kristo kwa dhati na kwa kuwajibika zaidi. Tunaweza kuiita njia ya Maria. Ni njia ya kielelezo cha Bikira wa Nazareti, mwanamke wa imani, wa kimya na wa usikivu. Ni pia njia ya ibada ya Kimaria inayohuishwa na hakika ya fungamano la moja kwa moja kati ya Kristo na Mama yake mtakatifu sana: kwa namna fulani, mafumbo ya Kristo ni pia mafumbo ya Mama, hata pale asipohusika moja kwa moja, kutokana na kwamba Maria aliishi ndani ya Yesu na kwa ajili yake. Katika Salamu Maria tukijitwalia maneno ya malaika Gabrieli na ya mtakatifu Elizabeti, tunajisikia msukumo wa kumtafuta upya daima kwa Maria, katika mikono yake na katika moyo wake, yule «mzao wa tumbo lake aliyebarikiwa» (taz. Lk 1:42).
 

Fumbo la Kristo, 'fumbo' la binadamu

 
25. Katika ushuhuda niliokwishataja kwamba niliutoa mwaka 1978 kuwa Rozari ndiyo sala yangu pendevu kuliko zote, nilitokeza wazo ambalo nataka kulisisitiza.
Hapo nilisema kuwa «sala sahili ya Rozari inapiga madundo ya maisha ya binadamu». Kwa mwanga wa tafakuri za hapa juu kuhusu mafumbo ya Kristo, si vigumu kuchimba uhusiano huo wa Rozari na ubinadamu. Uhusiano huo ni wa msingi kuliko unavyoonekana mara moja. Anayetulia katika kumkazia macho Kristo kwa kufuata hatua za maisha yake, hawezi kukosa kukuta ndani mwake ukweli kuhusu binadamu pia. Ndio tamko kuu la Mtaguso wa pili wa Vatikano, ambalo nimelifundisha mara nyingi kuanzia barua rasmi Redemptor Hominis: «Kwa kweli, fumbo la binadamu linaeleweka vizuri katika fumbo la Neno aliyefanyika mwili tu». Rozari inasaidia kujiandaa kupokea mwanga huo. Kwa kufuata safari ya Kristo, ambamo safari ya binadamu «imejumlishwa», imefunuliwa na kukombolewa, mwamini anajiweka mbele ya sura ya mtu halisi. Akikazia macho kuzaliwa kwake anajifunza uhai ulivyo mtakatifu, akitazama nyumba ya Nazareti anajifunza ukweli asili kuhusu familia kadiri ya mpango wa Mungu, akimsikiliza Mwalimu katika mafumbo ya maisha ya hadhara anapokea mwanga ili kuingia katika Ufalme wa Mungu na, akimfuata katika njia ya Kalivari, anajifunza maana ya uchungu kwa wokovu. Hatimaye, akiwakazia macho Kristo na Mama yake katika utukufu, anaona lengo ambalo kila mmoja ameitiwa, akikubali kuponywa na kugeuzwa sura na Roho Mtakatifu. Hivyo tunaweza kusema kuhusu kila fumbo la Rozari kwamba, likizingatiwa vizuri, linaangaza fumbo la binadamu.
Wakati huohuo, inamtokea mtu, hata bila ya kukusudia, kuleta kwenye mkutano huo na utu mtakatifu wa Mkombozi matatizo, mafadhaiko, kazi na mipango mingi ambayo inaathiri maisha yetu. «Umtwike Bwana mzigo wako naye atakutegemeza » (Zab 56:22). Kutafakari kwa njia ya Rozari ni kukabidhi mahangaiko yetu kwa mioyo yenye huruma ya Kristo na Mama yake. Miaka ishirini na tano baadaye, nikikumbuka majaribu ambayo sijayakosa katika kutimiza huduma ya Petro, najisikia kusisitiza, kama mwaliko wa dhati kwa wote wa kujipatia mang’amuzi hayo, kwamba kweli Rozari «inapiga madundo ya maisha ya binadamu», ili yalingane na madundo ya maisha ya Mungu, katika ushirika mfurahivu na Utatu mtakatifu, lengo na shauku ya maisha yetu.
 
 
 
 
 

SURA YA TATU

 
KWANGU MIMI KUISHI NI KRISTO
 
 
 

Rozari, njia ya kulishiza fumbo

 
26. Kutafakari mafumbo ya Kristo kunapendekezwa katika Rozari kwa mbinu maalumu, ambayo kwa maumbile yake inafaa kusaidia kuyalishiza. Ni mbinu ambayo msingi wake ni kukariri. Hiyo ni kweli kwanza kwa Salamu Maria, inayorudiwa mara kumi kwa kila fumbo. Tukitazama kijujuu tendo hilo la kukariri, tunaweza tukashawishika kuona Rozari ni kazi kavu na ya kukinaisha. Kumbe inawezekana kuitathmini tasbihi tofauti sana tukiiona kama tokeo la upendo usiochoka kumrudia mpenzi kwa maneno mengi yaliyojaa hisia ambayo, ingawa yanaonekana kufanana, ni mapya daima kutokana na hizo hisia unaoyajaa.
Katika Kristo, Mungu ametwaa kweli «moyo wa nyama». Yeye hana tu moyo wa Kimungu, uliojaa huruma na msamaha, bali pia moyo wa kibinadamu, unaoweza kupata mitikisiko yote ya mapendo. Tungehitaji ushuhuda wa Injili kuhusu jambo hilo, isingekuwa vigumu kuukuta katika majibizano ya kugusa kati ya Kristo na Petro baada ya ufufuko: «Je, Simoni wa Yohane, wewe wanipenda?». Swali hilo liliulizwa hata mara tatu, na jibu vilevile lilitolewa hata mara tatu: «Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda» (taz. Yoh 21:15-17). Mbali ya maana maalumu ya ukurasa huo, ulio muhimu sana kwa utume wa Petro, hakuna anayekosa kuona uzuri wa kuyarudia hayo mara tatu, ambapo sisitizo la swali na la jibu lake linajitokeza kwa maneno yanayojulikana sana na mang’amuzi ya daima ya upendo wa binadamu. Ili tuielewe Rozari, ni lazima tuingie katika mwendo wa saikolojia maalumu ya upendo.
Jambo moja ni wazi: ikiwa marudio ya Salamu Maria yanamlenga moja kwa moja Maria, tendo la upendo linamuendea hasa Yesu, pamoja na Maria na kwa njia yake. Marudio yanalishwa na hamu ya kujilinganisha na Kristo kikamilifu zaidi na zaidi, ambako ndio 'mpango' halisi wa maisha ya Kikristo. Mtume Paolo alitamka mpango huo kwa maneno ya moto: «Kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida» (Fil 1:21). Tena: «Ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu» (Gal 2:20). Rozari inatusaidia kukua katika kujilinganisha hivyo hadi lengo la utakatifu.
 
Mbinu ya kufaa...
 
27. Si ajabu kwamba fungamano na Kristo liweze kufaidika na msaada wa mbinu fulani pia. Mungu anajishirikisha kwa binadamu akiheshimu maumbile yetu na mwendo wa maisha. Ndiyo sababu maisha ya Kiroho ya Kikristo, ingawa yanaweza yakafikia namna za juu zaidi za kimya cha kuzama katika mafumbo, ambapo picha zote, maneno na matendo yote yanaachwa nyuma kutokana na nguvu ya muungano usiosemekana wa mtu na Mungu, hata hivyo kwa kawaida ni sifa yake kumhusisha mtu mzima katika maumbile yake changamano ya roho na mwili na katika mafungamano yake na wengine.
Hiyo inaonekana wazi katika liturujia. Sakramenti na visakramenti vimeundwa na mfululizo wa vitendo ambavyo vinahusisha pande mbalimbali za nafsi yetu. Hata sala isiyo ya liturujia inatokeza haja hiyohiyo. Hiyo inathibitishwa na kwamba huko Mashariki sala maalumu zaidi ya tafakuri ya Kikristo, ambayo kiini chake ni maneno: «Yesu, Kristo, Mwana wa Mungu, Bwana, unihurumie mimi mkosefu», inaendana kimapokeo na mwendo wa kupumua, ambao, wakati unaposaidia kudumu katika dua, unahakikisha uzito kama wa kimwili kwa hamu ya kumfanya Kristo awe pumzi, roho na 'yote' ya maisha.
 
... ambayo hata hivyo inaweza kuboreshwa
 
28. Katika barua ya kitume Novo Millennio Ineunte nilikumbusha kwamba leo, huku Magharibi pia, inasikika haja mpya ya kutafakari, ambako pengine katika dini nyingine kuna namna za kuvutia.  Hawakosekani Wakristo ambao, kwa kutojua vya kutosha mapokeo ya Kikristo ya kuzama katika mafumbo, wanakubali kushawishiwa na mapendekezo hayo. Lakini mara nyingi hayo kwa ndani msingi wake ni mawazo yasiyokubalika, hata kama yana mambo mazuri ambayo yanaweza yakapatana na mang’amuzi ya Kikristo. Katika mang’amuzi ya dini hizo pia zinatumika sana mbinu ambazo, zikilenga roho ijikusanye kwa dhati, zinahusisha nafsi na mwili, zinakariri maneno na kutumia ishara. Rozari inajipanga katika fremu hiyo ya kimataifa ya mang’amuzi ya kidini, lakini inajibainisha kwa sifa za pekee zinazolingana na madai maalumu ya Ukristo.
Kwa kweli Rozari ni mbinu tu mojawapo ya kuzama katika mafumbo. Ikiwa ni mbinu inatakiwa kutumika kuhusiana na lengo, isigeuke yenyewe kuwa lengo. Hata hivyo, ikiwa ni tunda la mang’amuzi ya karne kadhaa, mbinu yenyewe inatakiwa kuthaminiwa vya kutosha. Upande wake yanasimama mang’amuzi ya watakatifu wengi. Lakini hayo hayamaanishi kwamba haiwezi kuboreshwa. Ndipo unapolenga ukamilisho wa mifululizo ya mafumbo kwa mfululizo mpya wa mysteria lucis, pamoja na mashauri kadhaa kuhusu namna ya kusali ambayo nayapendekeza katika barua hii. Kwa njia yake sitaki kuvuruga muundo wa sala hiyo ulioimarika sana, bali kusaidia waamini kuuelewa upande wa ishara kulingana na mahitaji ya maisha ya kila siku. Pasipo hilo hatari siyo tu kwamba Rozari itashindwa kuzaa matunda ya Kiroho yanayotarajiwa, bali pia kwamba tasbihi inayotumika kwa kawaida kuisalia itakuja kutazamwa kama aina ya hirizi au chombo cha kishirikina kwa kupotosha kabisa maana yake na kazi yake.
 

Kutaja fumbo

 
29. Kutaja fumbo, na kwa wakati huohuo afadhali kupata nafasi ya kukazia macho picha inayolionyesha, ni kama kuweka wazi mpangilio wa tukio la kulizingatia. Maneno yanaongoza ubunifu na roho kwenye tukio maalumu au nafasi ya maisha ya Kristo. Katika maisha ya Kiroho yaliyostawi ndani ya Kanisa, heshima kwa picha takatifu na vilevile ibada mbalimbali zilizohusisha sana hizi za watu, tena na mbinu ile iliyopendekezwa na mtakatifu Ignasi wa Loyola katika Mazoezi ya Kiroho, zimetumia macho na ubunifu (compositio loci), zikiviona kama msaada mkubwa kwa kukusanya roho katika fumbo. Tena mbinu hiyo inalingana na mantiki yenyewe ya umwilisho: Mungu amependa kutwaa katika Yesu sura ya binadamu. Ni kwa njia ya ukweli wa mwili wake kwamba sisi tunaelekezwa kufungamana na fumbo lake la Kimungu.
Haja hiyo ya mambo ya kushikika inaitikiwa pia na kule kutaja mafumbo mbalimbali ya Rozari. Bila ya shaka hayo hayashiki nafasi ya Injili wala hayakumbushi kurasa zake zote. Kwa hiyo Rozari haishiki nafasi ya lectio divina, bali inaidai na kuistawisha. Lakini ikiwa mafumbo yanayozingatiwa katika Rozari, yakiwa ni pamoja na ukamilisho wake kwa mysteria lucis, yanaishia katika mambo makuu ya maisha ya Kristo, kutokana nayo roho inaweza kwa urahisi zaidi kuenea katika sehemu nyingine za Injili, hasa Rozari inaposaliwa katika nafasi maalumu za kujikusanya kirefu zaidi.
 

Kusikiliza Neno la Mungu

 
30. Ili tafakuri ipewe msingi wa Kibiblia na udhati mkubwa zaidi, inafaa baada ya kutaja fumbo kuwe na tangazo la dondoo la Biblia linalohusika ambalo linaweza kuwa refu kadiri ya hali. Kwa kuwa maneno mengine hayafikii kamwe nguvu maalumu ya Neno lililovuviwa na Mungu. Hilo linatakiwa kusikilizwa kwa hakika ya kwamba ni Neno lake lililotamkwa kwa ajili ya leo na «kwa ajili yangu».
Likipokewa hivyo, linaingia katika mbinu ya kukariri ya Rozari bila ya kusababisha ukinaifu unaoweza ukatokana na kukumbusha tu habari inayojulikana sana. Hapana, kazi si kukumbuka habari, bali kuacha Mungu ‘aseme’. Katika nafasi fulani ya fahari na ya kijumuia inaweza ikafaa Neno hilo lifafanuliwe kifupi.
 

Kimya

 
31. Usikivu na tafakuri vinajilisha kimya. Inafaa kwamba, baada ya kutaja fumbo na kutangaza Neno, tutulie kwa muda wa kufaa ili kulikazia macho fumbo la kufikiriwa, kabla hatujaanza sala ya midomo. Kuvumbua upya thamani ya kimya ni siri mojawapo ya utekelezaji wa sala hasa na wa tafakuri. Kati ya kasoro za jamii iliyotawaliwa na teknolojia na vyombo vya habari, mojawapo ni kwamba kimya kinazidi kuwa kigumu. Kama vile katika liturujia zinapendekezwa nafasi za kimya, hata katika kusali Rozari inafaa nafasi fupi ya kutulia baada ya kulisikiliza Neno la Mungu, wakati roho inapolenga yaliyomo katika fumbo maalumu.
 
«Baba Yetu»
 
32. Baada ya kusikiliza Neno na kulenga fumbo, hakuna budi kujiinua kwa Baba. Yesu, katika kila fumbo lake, anatufikisha daima kwa Baba, anayemuelekea mfululizo, kwa kuwa ametulia 'kifuani' pake (taz. Yoh 1:18). Yeye anataka kutuingiza katika urafiki wa dhati na Baba, ili tuseme pamoja naye «Aba!, Baba» (Rm 8:15; Gal 4:6). Ni katika uhusiano na Baba kwamba yeye anatufanya kuwa ndugu zake na ndugu sisi kwa sisi, akitushirikisha Roho ambaye ni wa kwake na wa Baba kwa pamoja. Sala ya Baba Yetu, ikiwekwa kama msingi fulani wa tafakuri juu ya Kristo na Maria inayostawi kwa njia ya kukariri Salamu Maria, inafanya tafakuri hiyo ya fumbo kuwa mang’amuzi ya Kikanisa hata inapofanyika upwekeni.
 
«Salamu Maria» kumi
 
33. Ndiyo sehemu kubwa zaidi ya Rozari na papohapo ndiyo inayoifanya iwe sala ya Kimaria kwa namna ya pekee. Lakini ikieleweka vizuri Salamu Maria yenyewe inaonyesha wazi kwamba sifa hiyo ya Kimaria haipingani na sifa ya Rozari kuwa sala ya Kikristo, bali inaisisitiza na kuikuza. Kwa kuwa sehemu ya kwanza ya Salamu Maria, inayotokana na maneno ambayo Maria aliambiwa na malaika Gabrieli na mtakatifu Elizabeti, ni kuzama kwa ibada katika fumbo lililofanyika katika Bikira wa Nazareti. Tunaweza kusema yanatokeza mshangao wa mbingu na dunia na kwa namna fulani yanadokeza furaha ya Mungu mwenyewe akitazama uzuri wa kazi yake bora kuliko zote – umwilisho wa Mwana katika tumbo la kibikira la Maria -, kufuatana na mtazamo mfurahivu wa kitabu cha Mwanzo (taz. Mwa 1:31), na ile aina ya ono asili au «pathos ambayo Mungu, mwanzoni mwa uumbaji, aliitazama kazi ya mikono yake». Katika Rozari, kukariri Salamu Maria kunatushirikisha furaha hiyo ya Mungu: ni shangwe, ni mshangao, ni uvumbuzi wa muujiza mkubwa kuliko yote iliyofanyika katika historia. Ndivyo unavyotimia utabiri wa Maria: «Tokea sasa vizazi vyote wataniita mbarikiwa» (Lk 1:48).
Kiini cha Salamu Maria, na kama bawaba kati ya sehemu yake ya kwanza na ya pili, ni jina la Yesu. Pengine, katika kukariri harakaharaka, kiini hicho kinasahauliwa pamoja na uhusiano wake na fumbo la Kristo linalokaziwa macho. Lakini mkazo juu ya jina la Yesu na juu ya fumbo lake ndio unaobainisha matumizi ya Rozari yenye maana na ya kuzaa matunda. Paulo VI katika himizo la kitume Marialis Cultus alikumbusha tayari desturi inayofuatwa sehemu fulanifulani ili kutia maanani jina la Kristo, yaani kuliongezea maneno yanayodokeza fumbo linalotafakariwa. Ni desturi inayostahili sifa, hasa katika sala ya pamoja. Inatokeza kwa nguvu imani katika Kristo ikiihusisha na nafasi mbalimbali za maisha ya Mkombozi. Ni ungamo la imani na, kwa wakati huohuo, inasaidia kudumisha uzingatifu wa tafakuri, ikiwezesha kulishiza fumbo la Kristo kadiri ya lengo la kukariri Salamu Maria. Kukariri jina la Yesu – jina pekee ambalo linatunawezesha kutumaini wokovu (taz. Mdo 4:12) – pamoja na lile la Mama yake mtakatifu sana, na kama kwa kuacha Maria awe ndiye anayelipendekeza kwetu, ni safari ya kulishiza inayolenga kutuingiza kwa dhati zaidi na zaidi katika maisha ya Kristo.
Kutokana na fungamano lake la pekee kabisa na Kristo, linalomfanya Maria awe Mama wa Mungu, Theotokos, inapata nguvu ile dua ambayo tunamuelekea katika sehemu ya pili ya sala, tukiyakabidhi maombezi yake ya kimama maisha yetu na saa ya  kufa kwetu.
 
«Atukuzwe»
 
34. Kuutukuza Utatu ndio lengo la sala hasa ya Kikristo. Kwa kuwa Kristo ndiye njia inayotufikisha kwa Baba katika Roho. Tukiifuata mpaka mwisho tunajikuta mfululizo mbele ya fumbo la nafsi tatu za Kimungu ambazo tuzisifu, tuziabudu na kuzishukuru. Ni muhimu kwamba Atukuzwe, kilele cha kuzama katika mafumbo, iwekwe mahali pa pekee katika Rozari. Katika sala ya hadhara inaweza kuimbwa ili kusisitiza kwa namna ya kufaa mtazamo huo wa msingi ulio maalumu wa kila sala ya Kikristo.
Kadiri tafakuri juu ya fumbo ilivyokuwa zingatifu, ya dhati na kuhuishwa na upendo kwa Kristo na kwa Maria – Salamu baada ya Salamu – basi kuutukuza Utatu mwishoni mwa makumi, badala ya kuwa hatima fupi tu, kunapata tuni yake halisi ya kuzama katika fumbo, kama kwa kuinua roho hadi juu mbinguni na kutufanya kwa namna fulani tupate sisi pia mang’amuzi ya Tabori, utangulizi wa kuzama kesho katika fumbo: «Ni vizuri sisi kuwapo hapa» (Lk 9:33).
 

Sala ya mwisho

 
35. Katika kawaida ya Rozari, baada ya kuutukuza Utatu inafuata antifona iliyo tofauti kadiri ya desturi. Bila ya kupunguza thamani ya maombi hayo, inafaa tuseme kuwa kuzama katika mafumbo kunaweza kutokeza vizuri zaidi uwezo wake wa kuzaa matunda kukiwa na mbinu ya kumalizia kila fumbo kwa sala ambayo ilenge kupata matunda maalumu ya tafakuri ya fumbo husika. Hivyo Rozari itaweza kutokeza kwa nguvu zaidi uhusiano wake na maisha ya Kikristo. Kufanya hivyo kunapendekezwa na sala nzuri ya liturujia inayotualika kuomba kwamba kwa kutafakari mafumbo ya Rozari, tuweze «kuiga yaliyomo na kupata yanayoahidi».
Hiyo sala ya mwisho inaweza kufuata namna tofauti halali, kama inavyotokea tayari. Hivyo Rozari inapata pia sura ya kulingana zaidi na mapokeo mbalimbali ya Kiroho na jumuia mbalimbali za Kikristo. Katika mtazamo huo, inatarajiwa kwamba yaenee kadiri ya busara ya kichungaji mapendekezo ya maana zaidi, afadhali kisha kujaribiwa katika vituo na patakatifu pa Maria ambapo sala ya Rozari inazingatiwa zaidi, hivi kwamba Taifa la Mungu liweze kufaidika na utajiri wowote halisi wa Kiroho, likiufanya uwe lishe kwa sala yake hasa.
 

Tasbihi

 
36. Chombo cha mapokeo cha kusalia Rozari ni tasbihi. Katika matumizi ya kijuujuu zaidi inaishia mara nyingi kuwa kifaa tu cha kuhesabia Salamu Maria zinazofuatana. Lakini inafaa pia kutokeza ishara inayoweza kuchangia tena kuzama katika mafumbo. Kuhusu jambo hilo, neno la kwanza la kusema ni kuwa tasbihi inamuelekea Msulubiwa, ambaye kwa namna hiyo anafungua na kufunga njia yenyewe ya sala. Maisha na sala ya waamini kiini chake ni Kristo. Yote yanatoka kwake, yote yamamlenga yeye, yote kwa njia yake, katika Roho Mtakatifu, yanamfikia Baba.
Kama chombo che kuhesabia, kinachoonyesha maendeleo ya sala, tasbihi inadokeza safari isiyokwisha ya sala hasa na ya ukamilifu wa Kikristo. Mwenye heri Bartolo Longo aliiona pia kama ‘mnyororo’ inayotuunganisha na Mungu. Naam, mnyororo, lakini mtamu; ndivyo unavyojidhihirisha daima uhusiano na Mungu aliye Baba. Mnyororo ‘wa kitoto’, unaotulinganisha na Maria, «mjakazi wa Bwana» (Lk 1:38), na, kimsingi zaidi, na Kristo mwenyewe ambaye, ingawa ni Mungu, alijifanya «mtumishi» kwa kutupenda. (Fil 2:7).
Ni vizuri pia kueneza maana ya kiishara ya tasbihi upande wa mafungamano kati yetu wenyewe, tukikumbuka kwa njia yake uhusiano wa ushirika na udugu unaotuunganisha wote na Kristo.
 

Mwanzo na mwisho

 
37. Kwa sasa katika mazingira tofauti ya Kanisa kuna namna mbalimbali za kuanza Rozari. Katika maeneo kadhaa kawaida ni kuanza na dua ya Zaburi 70: «Ee Mungu, uniokoe, Ee Bwana, unisaidie hima», kama kwa kuchochea ndani ya anayesali hakika nyenyekevu ya unyonge wake; kumbe pengine mwanzo unafanyika kwa kutamka maneno ya Nasadiki, kama kwa kuweka ungamo la imani kuwa msingi wa safari ya sala inayoanza. Namna hizo na nyinginezo ni halali vilevile kadiri zinavyoandaa roho kuzama katika mafumbo. Halafu sala inafungwa na ombi kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu, ili kupanua mtazamo wa anayesali hadi upeo mkubwa wa mahitaji ya Kanisa. Ni kwa ajili ya kuhamasisha mtazamo huo wa Kikanisa wa Rozari, kwamba Kanisa limeamua kuitajirisha kwa rehema takatifu kwa manufaa ya anayeisali kwa misimamo yanayotakiwa.
Kwa kweli, Rozari ikisaliwa hivyo inakuwa kwa hakika safari ya Kiroho ambamo Maria anajifanya Mama, mwalimu, kiongozi na kumtegemeza mwamini kwa maombezi yake ya nguvu. Haiwezekani kushangaa kwamba roho, mwishoni mwa sala hiyo, ambapo imeng’amua kwa dhati umama wa Maria, inajisikia haja ya kumsifu Bikira mtakatifu kwa sala nzuri ajabu ya Salamu Malkia na kwa Litania ya Loreto. Ni kilele cha safari ya ndani iliyomleta mwamini karibu sana na fumbo la Kristo na la Mama yake mtakatifu sana.
 
Mgawanyo katika siku za wiki
 
38. Rozari inaweza kusaliwa nzima kila siku, na wapo ambao wanafanya hivyo na kustahili sifa. Hivyo inakuja kujaza kwa sala siku za waaamini wengi waliojitosa kusali tu, au inakuja kuongozana na wagonjwa na wazee ambao wana muda mwingi usio na shughuli. Lakini ni wazi kwamba – hasa ukiongezwa mfululizo mpya wa mysteria lucis – wengi hawataweza kusali zaidi ya sehemu moja, kadiri ya mpangilio fulani katika wiki. Mgawanyo huo katika juma unazipatia siku za wiki ‘rangi’ fulani ya Kiroho, kidogo kama liturujia inavyofanya na vipindi mbalimbali vya mwaka wa Kanisa.
Kadiri ya desturi ya sasa, Jumatatu na Alhamisi zinatumika kutafakari «mafumbo ya furaha», Jumanne na Ijumaa «mafumbo ya uchungu», halafu Jumatano, Jumamosi na Jumapili «mafumbo ya utukufu». Tuingize wapi «mafumbo ya mwanga»? Tukizingatia kwamba mafumbo ya utukufu yanapendekezwa mfululizo Jumamosi na Jumapili, na kwamba kimapokeo Jumamosi ni siku ya Maria hasa, inafaa kushauri kuhamishia Jumamosi tafakuri ya pili ya wiki juu ya mafumbo ya furaha, ambamo uwepo wa Maria unajitokeza. Hivyo Alhamisi inabaki na nafasi kwa kutafakari mafumbo ya mwanga.
Hata hivyo elekezo hilo halikusudii kuzuia uhuru wa kufaa katika kutafakari kwa mtu mmojammoja au kijumuia, kadiri ya mahitaji ya Kiroho na ya kichungaji na hasa kadiri ya kutukia siku za liturujia ambazo zinaweza zikashauri kurekebisha mpangilio huo kwa namna ya kufaa. Kilicho muhimu kweli ni kwamba Rozari itazamwe na kung’amuliwa zaidi na zaidi kama safari ya kuzama katika mafumbo. Kwa njia yake na kwa kukamilishana na kazi ya liturujia, juma la Mkristo linalotegemea Siku ya Bwana, siku ya ufufuko, linakuwa safari kupitia mafumbo ya maisha ya Kristo, naye anajitokeza katika maisha ya wanafunzi wake kuwa ndiye Bwana wa nyakati na wa historia.
 

 

 

 

 

HATIMA

 

«Rozari mbarikiwa wa Maria, mnyororo mtamu unaotuunganisha na Mungu»
 
39. Tuliyoyasema mpaka sasa yanatokeza sana utajiri wa sala hiyo ya kimapokeo ambayo ina usahili wa sala ya watu wadogo, lakini pia udhati wa kiteolojia wa sala inayowafaa wanaojisikia haja ya sala iliyokomaa zaidi.
Daima Kanisa limekiri kwamba sala hiyo ina nguvu ya pekee, likiyakabidhi matumizi yake ya pamoja na ya kudumu mambo magumu zaidi. Wakati ambapo Ukristo wenyewe ulikuwa hatarini, Kanisa liliona kwamba nguvu ya sala hiyo ndiyo iliyoepusha janga, na Bikira wa Rozari alisalimiwa kama mwombezi wa wokovu huo.
Leo naikabidhi kwa radhi nguvu ya sala hiyo – kama nilivyodokeza mwanzoni – kipeo cha amani duniani na kile cha familia.
 

Amani

 
40. Matatizo yanayojitokeza katika upeo wa ulimwengu mwanzoni mwa milenia mpya yanatufanya tufikirie kwamba kazi kutoka Juu tu, yenye uwezo wa kuelekeza mioyo ya wanaoishi katika nafasi za kushindana na ya wanaoshika mikononi mwao kesho ya mataifa, inaweza kutumainisha kwamba kesho hiyo haitakuwa na magiza makubwa kama ya sasa.
Rozari ni sala ambayo kwa maumbile yake inalenga amani, kwa sababu ni kumkazia macho Kristo, Mfalme wa amani na «amani yetu» (Ef 2:14). Anayelifanya fumbo la Kristo kuwa lake pia – na ndilo lengo hasa la Rozari -, anajifunza siri ya amani na kuigeuza kuwa mpango wa maisha. Tena, kutokana na tabia yake kama tafakuri, pamoja na mfuatano wake mtulivu wa Salamu Maria, Rozari inamtuliza anayesali na kumuandaa kupokea na kung’amua ndani kabisa mwa nafsi yake, halafu kueneza kandokando yake, ile amani halisi ambayo ni zawadi maalumu ya Mfufuka (taz. Yoh 14:27; 20:21).
Pia ni sala ya amani kutokana na matunda ya upendo inayoyazaa. Ikisaliwa vizuri kama tafakuri halisi, Rozari, kwa kurahisisha mkutano na Kristo katika mafumbo yake, inatambulisha pia uso wa Kristo katika ndugu, hasa wanaoteseka zaidi. Inawezekanaje kulikazia macho, katika mafumbo ya furaha, fumbo la Mtoto aliyezaliwa Bethlehemu bila ya kujisikia hamu ya kupokea, kutetea na kustawisha uhai, kwa kubeba mateso ya watoto sehemu zote za dunia? Inawezekanaje kufuata nyayo za Kristo mfunuaji wa ukweli, katika mafumbo ya mwanga, bila ya kuazimu kutoa ushahidi wa Heri zake katika maisha ya kila siku? Tena inawezekanaje kumkazia macho Kristo aliyelemewa na msalaba na kusulubiwa, bila ya kujisikia haja ya kumsaidia kama «Wakirene» wake katika kila ndugu aliyevunjwa na uchungu au kulemewa na hali ya kukata tamaa? Hatimaye, inawezekanaje kuukazia macho utukufu wa Kristo mfufuka na wa Maria aliyetawazwa Malkia, bila ya kujisikia hamu ya kufanya ulimwengu huu uwe mzuri zaidi, wenye haki zaidi na kulingana zaidi na mpango wa Mungu?
Basi, Rozari huku ikitufanya tumkazie macho Kristo, inatufanya pia wajenzi wa amani duniani. Kwa sifa yake ya kuwa dua inayosisitizwa na ya pamoja, kulingana na mwaliko wa Kristo wa kusali «sikuzote» bila ya kukata tamaa (Lk 18:1), inatuwezesha kutumaini kwamba, leo pia 'pambano' gumu kama lile la amani linaweza kupata ushindi. Mbali na kukimbia matatizo ya ulimwengu, Rozari inatusukuma hivyo kuyatazama kwa macho ya uwajibikaji na ya ukarimu, na inatupatia nguvu ya kuyakabili tukiwa na hakika ya kupata msaada wa Mungu na nia imara ya kuushuhudia katika nafasi yoyote «upendo, ndio kifungo cha ukamilifu» (Col 3:14).
 
Familia: wazazi
 
41. Rozari, pamoja na kuwa sala kwa ajili ya amani, tangu mwanzo ni pia sala ya familia na kwa ajili ya familia. Zamani sala hiyo ilipendwa sana na familia za Kikristo, na bila ya shaka ilichangia umoja wake. Ni lazima tusitapanye urithi huo wa thamani. Ni lazima turudi kusali katika familia na kusali kwa ajili ya familia, kwa kutumia tena namna hii ya kusali.
Ikiwa katika barua ya kitume Novo Millennio Ineunte nilihimiza Liturujia ya Vipindi liadhimishwe na walei pia katika maisha ya kawaida ya jumuia za parokia na za vyama mbalimbali vya Kikristo, nataka kufanya vilevile kuhusu Rozari. Ni njia mbili za sala hasa ya Kikristo, si za kuchagua kati yake, bali za kukamilishana. Hivyo naomba wanaoshughulikia uchungaji wa familia wahamasishe kwa moyo sala ya Rozari.
Familia inayosali kwa umoja, inadumu kuwa na umoja. Kwa mapokeo ya muda mrefu, Rozari takatifu inafaa kwa namna ya pekee kuwa sala inayokusanya familia. Wanafamilia, kwa kumkazia macho Yesu, wanajipatia upya uwezo wa kutazamana daima usoni ili kuelewana, ili kushikamana, ili kusameheana, ili kuanza upya kwa agano la upendo lililofanywa upya na Roho wa Mungu.
Matatizo mengi ya familia za kisasa, hasa katika jamii zilizoendelea kiuchumi, yanatokana na kwamba inazidi kuwa vigumu kushirikishana. Kukaa pamoja kunashindikana, na huenda nafasi chache za kukaa pamoja zikajazwa na picha za televisheni. Kuanza upya kusali Rozari katika familia ni kuingiza katika maisha ya kila siku picha tofauti sana, zile za fumbo linalookoa: picha ya Mkombozi, picha ya Mama yake mtakatifu sana. Familia ambayo inasali pamoja Rozari inaiga kidogo mazingira ya nyumba ya Nazareti: Yesu anawekwa katikati, kwa kushiriki pamoja naye furaha na uchungu, kwa kumkabidhi mikononi mahitaji na matarajio, kwa kuchota kwake tumaini na nguvu ya kuendelea na safari.
 
... na watoto
 
42. Ni pia jambo zuri na la kufaa kuikabidhi sala hiyo safari ya kukua kwa watoto. Je, Rozari si safari ya maisha ya Kristo, tangu kutungwa mpaka kufa, hadi kufufuka na utukufu? Leo inazidi kuwa vigumu kwa wazazi kuwafuata watoto katika hatua mbalimbali za maisha. Katika jamii ya teknolojia iliyostawi, ya vyombo vya upashanaji habari na ya utandawazi, yote yamekuwa yanakwenda haraka sana, na umbali wa kiutamaduni kati ya vizazi unazidi kukua. Mapema aina yoyote ya ujumbe na mang’amuzi yasiyotarajiwa yanapata nafasi katika maisha ya watoto na vijana, hivi kwamba pengine wazazi wanafadhaika kuwaepusha na hatari wanazokabiliana nazo. Si kwa nadra wanapatwa na hali ya kuvunjika moyo kabisa, wakiona wanao walivyoshindwa na udanganyifu wa dawa za kulevya, na mivuto ya anasa isiyo na mipaka, na vishawishi vya ukatili, na aina mbalimbali za matendo yanayotokeza mtu asivyoona maana ya maisha na alivyokata tamaa.
Kusali Rozari kwa ajili ya watoto, tena afadhali pamoja na watoto, kwa kuwalea tangu utotoni kuwa na nafasi hiyo ya «kutulia kwa sala» kifamilia kila siku, bila ya shaka si utatuzi wa matatizo yote, lakini ni msaada wa Kiroho wa thamani. Inawezekana kupinga kwa kusema Rozari inaonekana ni sala isiyofaa kuwaridhisha watoto na vijana wa leo. Lakini pengine hoja hiyo inategemea namna ya kusali ambayo mara nyingi si sahihi. Zaidi ya hayo, bila ya kupotosha muundo wake wa msingi, hakuna kinachozuia kwamba kwa watoto na vijana– katika familia kama vile katika vikundi - sala ya Rozari isitajirishwe na ishara na vitendo vya kufaa, ambavyo visaidie kuielewa na kufaidika nayo. Kwa nini tusijaribu? Kwa msaada wa Mungu, uchungaji wa vijana usiokata tamaa bali wenye bidii na ubunifu unaweza kufanya mambo ya maana kweli. Siku za Kimataifa za Vijana zimenionyesha kiasi gani! Rozari ikipendekezwa vizuri, nina hakika kuwa vijana wenyewe wataweza kuwashangaza tena wazee kwa kuifanya sala hiyo kuwa ya kwao na kuitumia kwa umotomoto maalumu wa umri wao.
 

Rozari, hazina ambayo tuivumbue upya

 
43. Wapendwa ndugu wa kiume na wa kike! Sala rahisi hivi, na kwa wakati huohuo tajiri hivi, inastahili kweli kuvumbuliwa tena na jumuia ya Kikristo. Tufanye hivyo hasa mwaka huu, tukipokea pendekezo hilo kama uimarishaji wa mpango uliochorwa katika barua ya kitume Novo Millennio Ineunte, ambayo programu za kichungaji za Makanisa maalumu mengi zimeifuata katika kupanga juhudi kwa miaka ya jirani.
Kwa namna ya pekee nawaelekea nyinyi, wapendwa ndugu katika uaskofu, mapadri na mashemasi, nanyi watenda kazi wa kichungaji katika huduma mbalimbali, ili kwa kung’amua wenyewe uzuri wa Rozari, muihamasishe kwa bidii.
Nawategemea nyinyi pia wanateolojia, ili kwa masomo yenu makini na ya hekima kwa wakati mmoja, yenye mzizi katika Neno la Mungu na usikivu kwa maisha halisi ya taifa la Wakristo, mtokeze misingi ya Kibiblia, utajiri wa Kiroho na nguvu ya kichungaji ya sala hiyo ya kimapokeo.
Nawategemea nyinyi, wanaume na wanawake mliowekwa wakfu, ambao mnaitwa kwa namna ya pekee kuukazia macho uso wa Kristo mkijifunza kwa Maria.
Nawaangalia nyinyi nyote, ndugu wa kiume na wa kike wa hali yoyote ya maisha, nyinyi, familia za Kikristo, nanyi wagonjwa na wazee, nanyi vijana: mshike upya mikononi kwa tumaini tasbihi ya Rozari, mkiivumbua upya katika mwanga wa Maandiko matakatifu, kulingana na liturujia, katika hali halisi ya maisha ya kila siku.
Mwaliko wangu huu usipotee bure! Mwanzoni mwa mwaka wa ishirini na tano wa upapa wangu, nakabidhi barua hii ya kitume mikononi mwa Bikira Maria mwenye hekima, nikisujudu Kiroho mbele ya picha yake iliyopo katika patakatifu pazuri ajabu ambapo mwenye heri Bartolo Longo, mtume wa Rozari, alipajenga kwa heshima yake. Najitwalia kwa radhi maneno yake ya kusisimua ambayo alifunga Dua maarufu kwa Malkia wa Rozari takatifu: «Rozari mbarikiwa wa Maria, mnyororo mtamu unaotuunganisha na Mungu, kiungo cha upendo kinachotuunganisha na Malaika, mnara wa wokovu dhidi ya mashambulizi ya toka motoni, bandari salama katika dhoruba iliyotupata sote, sisi hatutakuacha tena kamwe. Wewe utatufariji saa ya kufa. Kwako tutatoa busu la mwisho uhai utakapozimika. Na sauti ya mwisho ya midomo yetu itakuwa jina lako tamu, Malkia wa Rozari wa Pompei, Mama yetu mpendwa, kimbilio la wakosefu, Mtawala mfariji wa wenye huzuni. Uhimidiwe popote, leo na daima, duniani na mbinguni».
 
Kutoka Vatikano, tarehe 16 Oktoba mwaka 2002, mwanzo wa mwaka wa ishirini na tano wa Upapa wangu.

YOHANE PAULO II

nukuu: alfagems

No comments:

Post a Comment