Tuesday, April 3, 2012

BIBLIA YA KIJAPANI YAANZISHWA

Biblia ya Kijapan yakamilika
TOKYO, Japan
TUMSIFU YESU KRISTU ! 


KITUO cha Mafunzo ya Bilblia cha Wafransiskani cha Tokyo, nchini Japan kimechapisha toleo la ‘Kitabu cha Yeremiah’ katika Biblia kwa lugha ya Kijapan hatua ambayo inakamilisha tafsiri ya Biblia iliyofanyika katika awamu 37.
Kituo hicho cha mafunzo kijulikanacho kama, Furanshisukp-kai-Seisho, kinachoongozwa na Padre Odaka Takeshi, kimekamilisha kazi iliyoanzishwa mwaka 1956 na mkurugenzi aliyepita, Padre Bernardino Schneider, OFM, ambaye katika umri wa miaka 84, bado anajihusisha katika mradi huo.
Wazo la kutoa tafsiri hiyo liliibuka mwaka 1952, wakati Japan ikiwa bado inafanya ukarabati kutokana na madhara ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Mwaka huo Padre Schneider, mzaliwa wa Cincinnati, Ohio, aliwasili katika Tokyo kama mmisionari.
Inasemekana kuwa wakati huo toleo pekee lililokuwepo katika lugha ya Kijapan lilikuwa ni la Biblia ya Kilatini la Vulgate. Lilikuwa ni katika lugha ya Kijapan ya zamani ambayo vijana wa sasa wa Kijapan hawawezi kuiongea.
Tafsiri hiyo iliyoanzishwa na Padre Schneider iko katika Kijapan cha kuongea na imezingatia makala za hivi karibuni zinazokosoa tafsiri iliyotangulia. hata hivyo imehifadhi Biblia ya Vulgate katika lugha ya Kilatini.
Padre Takeshi alitangaza kuwa ndani ya miaka mitano ijayo kituo hicho kinatumaini kuchapisha tafsiri ya Biblia kamili katika kitabu kimoja.
Inasemekana kuwa toleo la mwisho la Biblia katika kitabu kimoja lilichapishwa katika miaka ya 1980 na Chama cha Biblia cha Japan katika mradi ambamo wanafunzi Wakatoliki na Waprotestanti walishiriki.

No comments:

Post a Comment